chikita

TANGAZA NASI

Saturday, January 2, 2016

ALSHABAB WAMSHAMBULIA TRUMP

Kundi la wapiganaji wa Al-Shabab kutoka Somalia limetoa kanda ya video ya propaganda ambayo imemtaja mgombea Urais wa Marekani bwana Donald Trump
Hii imejiri wiki kadha baada ya Trump, anayeongoza kinyang’anyiro cha kutafuta atakayepeperusha bendera ya chama cha Republican, kupendekeza Waislamu wazuiwe kuingia Marekani.
Kundi la al-Shabab, ambalo lina uhusiano na mtandao wa Al-Qaeda, linaelekeza ujumbe kwa Wamarekani weusi, likiwahimiza kusilimu na kushiriki kwenye Jihad au vita vitakatifu.
Kundi hilo linasema kwenye video hiyo kwamba ubaguzi wa rangi, ukatili wa polisi na chuki dhidi ya Waislamu vimesheheni Marekani.
Wasimamizi wa kampeni ya Bw Trump hawajazungumza lolote kuhusu video hiyo.
Miaka ya hivi karibuni, Wasomali-Wamarekani kutoka Minnesota wameripotiwa kwenda Somalia kujiunga na al-Shabab.
Chanzo: BBC

Monday, September 26, 2011

SIASA NA MAISHA

Mgombea Ubunge Jimbo la Igunga kwa tiketi ya Cuf, Leopold Mahona (kulia) akicheza mchezo wa bao kwenye kijiwe kilichopo mtaa wa kijiji cha Mbutu, Wilaya Igunga, jana, ikiwa ni sehemu ya kampeni yake ya kuomba kura kwa wananchi wa jimbo hilo. Picha na Fidelis Felix

Monday, September 19, 2011

HIVI KWELI JAMANI BADO TUNAYAHITAJI HAYA KATIKA NCHI ZETU KARNE HII YA 21.????

Nghoboko Masele aliyejitambulisha kama balozi wa nyumba kumi kumi wa CCM, katika kijiji cha Mwayunge Mashariki Kata ya Igunga, akiwa chini ya ulinzi baada kukamatwa na wafuasi wa chadema akiorodhesha majina na namba za shahada za wapiga kura pamoja na namba za simu zao katika jiji hicho.jana. Picha na Fidelis Felix

Friday, September 16, 2011

UTAWALA PYA WA LIBYA WALAUMIWA

 
Shirika la kutetea haki za binaadamu la Amnesty International limesema kuwa baraza la mpito la Libya lichukue hatua kuzuia ukiukaji wa haki za binaadamu unaofanywa na wapiganaji wanaompinga Gaddafi. Katika ripoti yake mpya, shirika hilo linasema kuwa pamoja na kuwa vikosi vinavyomuunga Gaddafi ndiyo vimehusika na ukiukaji mkubwa wa haki za binaadamu, wapiganaji wanaompinga pia wamehusika katika mauaji na kutesa watu.
Mapema,Muammar Gaddafi alisisitiza katika ujumbe kupitia televisheni kuwa wataendelea na mapigano hadi "wapate ushindi".Kwa sasa haijulikani kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 69 yuko wapi.Habari zaidi zinasema kuwa, kiongozi wa baraza la mpito la Libya Mustafa Abdul Jalil ametoa hotuba yake ya kwanza kwa taifa mjini Tripoli tangu walipomuondoa Gaddafi, akitoa wito wa kuwa na taifa lenye msingi wa demokrasia ya kiislamu yenye mfumo wa ''kadri''.
Vikosi vinavyompinga Gaddafi vimesitisha mashambulio yake dhidi ya mji wa Bani Walid ambao unadhibitiwa na vikosi vinavyomuunga mkono Gaddafi. Waandishi wa habari wanasema walipata upinzani mkubwa kinyume na walivyotarajia.

BWANA NAPE NNAUYE KATIKA HEKAHEKA ZA KUPIGA KAMPENI LEO HUKO SINGIDA KATIKA UCHAGUZI MDOGO WA DIWANI

KATIBU WA ITIKADI NA UENEZI CCM BWN. NAPE NNAUYE

YAH:KUOMBA RADHI

Usiku wa kuamkia jumamosi ya tarehe 10 / 09 2011 tukio kubwa na la huzuni lilitokea huko Zanzibar ambapo wananchi wengi walipoteza maisha na wengine kujeruhiwa wakati walipopatwa na ajali ya kuzama kwa MELI iliyokuwa ikitoka Unguja kuelekea Pemba.

Kwa bahati mbaya siku hiyo ya Jumamosi taaasisi yetu ilikuwa inahitimisha Fainali za Taifa za Mashindano ya Urembo ya Miss Tanzania 2011.

Kama waandaaji wa Mashindano haya na wenye Mamlaka kamili ya maamuzi juu ya ama kuendelea au la kuahirisha jambo hili, tulipatwa na mshituko mkubwa sana juu ya tukio hilo.

kamati yetu ilikaa na kutakafari katika tukio hilo kwa kuzingatia mambo yafuatayo:-

• Taarifa kamili ya maafa haya tuliipata rasmi saa tisa na nusu mchana ( 9:30 ) siku ya jumamosi ambayo ilikuwa ni masaa machache kabla ya Fainali za Miss Tanzania kuanza katika ukumbi wa Mlimani City.

• Wenzetu wa TFF waliendelea na mechi za ligi kuu ikiwemo ya Yanga na Ruvu Shooting.

• Katika kumbi za starehe ikiwemo mabaa na burudani za muziki wa bendi na kumbi za disco ziliendelea kama kawaida.
• Muda uliokuwa umebaki kuwakilisha jina la mshiriki wetu kwenye fainali za Miss World zilikuwa zimekwisha hivyo kulikuwa na hatari ya kupoteza nafasi hiyo

• Pia tamko rasmi la kusimamisha shughuli zote za burudani lilianza tarehe 11 septemba 2011 kuomboleza Kitaifa maafa hayo.

Hata hivyo kama waandaaji tulifanya shindano tukiwa katika maombolezo kwani kabla ya kuanza shindano Watu wote waliokuwepo ukumbini walisimama kimya kwa dakika moja na hata washiriki walipoingia kwenye jukwaa kwa mara ya kwanza walikuwa wamevaa vitambaa vyeusi katika mikono yao ikiashilia maombolezo.

Hali hii imetupa mkanganyiko na kujikuta tukiendelea na mashindano kitu ambacho tunaona tumewakosea Watanzania wenzetu.

Kama Waandaaji tunapenda kusistiza kwamba tunawajibika kwa hayo yaliyotokea na si Taasisi yeyote au Kampuni yeyote na tunaomba ichukuliwe kama ni makosa ya kibinaadamu hasa ukizingatia mazingira magumu tuliyokuwa nayo kwa wakati huo na mkanganyiko wa matukio na taarifa za tatizo hilo.

KUOMBA RADHI
Hata hivyo shughuli hiyo inawezekana imewakwaza watu wengi na kwa sababu hiyo na pia hali halisi ya janga hilo na kwa niaba ya viongozi wenzangu na wadau wa shughuli zetu tunatoa tamko la dhati kwa Familia za ndugu wote walikumbwa na maafa haya, wale wote walionusurika katika ajali hii na Watanzania wote kwa ujumla, kwamba TUNAWAOMBA RADHI KWA MKANGANYIKO ULIOTUTOKEA HADI KUFIKIA HALI HII. Hatuna neno zaidi ya kusema na kusisitiza “TUNAOMBA RADHI”

Mwenyezi MUNGU aziweke roho za marehemu mahali pema peponi,
Amina,
Hashim Lundenga
Mkurugenzi

Sunday, September 4, 2011

DUUH LIYUMBA KIBOKO. AKAMATWA NA SIMU GEREZANI.


ALIYEKUWA Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi (DPA) wa Benki Kuu Tanzania (BoT), Amatus Liyumba ambaye anatumikia kifungo cha miaka miwili jela, ameingia matatani tena akidaiwa kukutwa na simu gerezani aliyoitumia kuwasiliana na Rais Jakaya Kikwete.

Liyumba kwa sasa anatumikia adhabu ya kifungo cha miaka miwili katika Gereza la Ukonga, baada ya kupatikana na hatia ya matumizi mabaya ya madaraka katika ofisi ya umma wakati wa akifanya kazi BoT.

Wakati bado akiwa anaendelea na adhabu hiyo, taarifa zilizopatikana jijini Dar es Salaam jana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile zilisema Liyumba alifikishwa katika Kituo cha Polisi cha Stakishari kilichopo Ukonga na kuhojiwa kwa kosa la kukutwa na simu gerezani.

Habari hizo zilifafanua kwamba Liyumba alifikishwa kituoni hapo saa 3:00 asubuhi kwa gari la Magereza lenye vioo vyeusi na kuhojiwa kwa muda wa takribani dakika 30 kuhusu tuhuma hizo.

Vyanzo hivyo vya habari vilifafanua kwamba, Liyumba anadaiwa kukutwa na simu ambayo ilibaki kituoni hapo kwa ushahidi.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Julai mwaka huu Liyumba alimpigia simu Rais Kikwete kwa kutumia simu hiyo. Hata hivyo, bado haijafahamika ni nini hasa alichomweleza Rais lakini habari zaidi zinadai kuwa kitendo hicho kilimfanya mkuu huyo wa nchi kuhoji iweje Liyumba amiliki simu wakati ni mfungwa?
Kutokana na tukio hilo, inadaiwa kuwa maofisa usalama walimwekea mtego na juzi usiku walimdaka akiwa na simu hiyo na asubuhi yake walimpeleka kituoni hapo kwa mahojiano.

WADAU WA JAHAZI LA CLOUDS FM WAKIPOZI KWA PICHA YA UKUMBUSHO

Ni Anold Kayanda, Wasiwasi Mwabulambo na Efraim Samson Kibonde watangazaji wa kipindi cha jahazi kinachopeperusha matangazo yake kila siku za Jumatatu hadi Ijumaa kupitia kituo cha clouds Fm cha jijini Dar es Salaam

Friday, September 2, 2011

JK HUWA ANAWATEMBELEA WAGONJWA


WASEMAVYO WACHAMBUZ

SERIKALI ya awamu ya nne iliingia madarakani na kauli mbiu ya “Maisha bora kwa kila Mtanzania.” Timu ya wana mtandao iliyoiingiza hii serikali ndani ya ikulu yetu, ilibobea katika uundaji wa kauli mbiu.
Itakumbukwa kuwa ni timu hiihii ya wana-mtandao iliyoibuka na kauli mbiu ya “Kasi mpya, Ari mpya na Nguvu mpya.” Hata baada ya mtandao kusambaratika, Rais Kikwete na mtandao masalia walikuja na kauli mbiu ya “Kasi zaidi, Ari zaidi na Nguvu zaidi.” Laiti mvuto wa kauli mbiu ungeendana na uhalisia; Watanzania tungekuwa mbali sana. 
Watu wengi hivi sasa wanakubaliana pasipo kutumia vigezo maalum kuwa, chini ya serikali ya awamu ya nne, hali mbaya imekuwa na kasi, ari na nguvu zaidi kuliko mambo mazuri.
Tamko hili bila vigezo linaweza kuonekana ni propaganda za kisiasa, lakini kwangu mimi kigezo kikuu ni waasisi wenyewe wa kauli mbiu hizi ambao nimeongea nao na wao wakakiri kuwa, “Mambo yamegeuka kinyume na walivyotarajia.”
Hata ukitumia kipengele kimoja tu cha thamani ya shilingi ya Tanzania ambacho ni mhimili mkuu wa shughuli zote za kiuchumi ndani ya nchi, ni rahisi kuona ukweli wa hoja yangu.
Wakati serikali hii inaingia madarakani mwaka 2005, thamani ya shilingi dhidi ya dola ilikuwa kati ya Sh. 1,000 na 1,100. Hivi sasa shilingi imeporomoka sana na muda si mrefu yaweza kuingia shilingi 2,000 kwa dola moja hata kabla ya mwisho wa mwaka huu; huku mfumoko wa bei ukipaa.
Kutokana na kuporomoka kwa thamani ya shilingi, wiki hii tumeshuhudia matangazo ya kiama kwa Watanzania. TANESCO wametangaza ongezeko la bei ya umeme wakati hata mgawo wenyewe haujaisha.
Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza ongezeko la bei ya mafuta ya taa, petroli na dizeli. Ongezeko la bei ya mafuta linakuja wakati ambapo hata baadhi ya vituo vya mafuta vilikuwa bado vikiendelea na mgomo wa kuuza nishati hiyo. Ongezeko hili halitegemewi kuondoa mgomo huo kwa sababu linatokana na kuporomoka kwa thamani ya shilingi.
Inaeleweka vema kuwa ongezeko la bei ya umeme na mafuta linaongeza moja kwa moja bei za bidhaa nyinginezo pamoja na huduma muhimu za kijamii. Haitarajiwi kuwa ongezeko hili litaongeza ubora wa huduma wala kuzisogeza karibu na watumiaji. Kimantiki, ongezeko la bei kwa huduma hizi, ni ongezeko la maumivu kwa watumiaji.
Kama nilivyodokeza hapo juu, mtiririko wa matukio yanayofanya maisha ya Watanzania kuwa magumu, ni kinyume na matarajio ya wahandisi/wajenzi wa mfumo wa utawala wa serikali ya sasa. Hata wao wanashangaa ni kwa nini mambo yanazidi kuwa magumu. Kinachokosekana ni tamko lao hadharani kuwa hali ni ngumu.
Wanasema na kusononeka mafichoni wakati Watanzania waliowaweka madarakani wanazidi kuumia. Kwa hali ya uchumi kugeuka na kuwa kinyume na matarajio ni jambo la kawaida katika mifumo ya uchumi.
Kilicho kigeni katika hali yetu, ni tabia ya watawala kushindwa kueleza wazi ni nini kimetokea na kufanya hali za Watanzania kuzidi kuwa mbaya kuliko zilivyokuwa kabla hawajaingia madarakani. Badala ya kusema ukweli, watawala wamekazana kutangaza kuwa uchumi unapaa na hali ya Watanzania ni bora!
Kwa sasa kauli mbiu inayofaa ni ile ya “Maisha mabaya kwa kila Mtanzania.” Haiwezekani kwamba watawala wetu hawa walikaa, wakapanga kuwa walete maisha mbaya kwa kila Mtanzania. Lakini kutokana na kimya chao, hisia zinaanza kujengeka miongoni mwa Watanzania kuwa yawezekana walipanga hivyo. Hisia hizi zikiachwa ziaminike, itakuwa vigumu kudhibiti ghadhabu ya wananchi dhidi ya serikali hii.
Awamu iliyopita ilikabidhi mustakabali wa uchumi wa taifa letu mikononi mwa wawekezaji. Serikali iliuza kila kitu na kufungua milango yote kwa wawekezaji. Matokeo ya sera hii, wote tumeyaona kwa masikitiko makubwa sana.
Watanzania wamegeuka kuwa wapangaji na wapagazi huku wageni wakiwa wamiliki wa njia kuu za uchumi. Rais Mkapa aliwahi kunukuliwa akisikitika kuwa hali hii hakuikusudia kwa sababu alidai yeye alilenga “kubinafsisha” siyo “kubinafasisha.”
Chini ya serikali ya Mkapa, wawekezaji walipata ushirikiano mzuri wa serikali na kuwekewa mazingira ya kunyonya raslimali zetu; lakini pia kulikuwa na mwanya fulani kwa baadhi ya wazawa kufaidi kupitia migongo ya wawekezaji hao.
Mazingira ya wawekezaji kwa sasa yamebadilika. Sera za uchumi wa taifa letu hazieleweki na zinazoeleweka hazifuatwi. Serikali inayoimba wimbo wa uchumi wa soko huria, hivi sasa imetumbukia katika mkakati wa udikteta unaotishia usalama wa mitaji ya wawekezaji kwa sababu hakuna umeme wa uhakika.
Aidha, hakuna uhuru kamili wa kuendesha soko huria, hakuna mazingira sawa ya ushindani na wala hakuna dalili za kukomesha rushwa na ukiritimba katika shughuli za kiuchumi.
Mzunguko mzima wa shughuli za uwekezaji umejaa rushwa kila hatua na kutegeana. Mmoja wa wawekezaji wazoefu hapa nchini amenieleza kuwa kila hatua analazimika kuonana na rais ili aweze kufanya shughuli zake kwa ufanisi!
Watanzania wameshuhudia mijadala ya ajabu bungeni kuhusiana na masuala ya uwekezaji na uendeshaji wa shughuli za biashara. Huku katika upande mmoja bunge likionekana wazi kuingilia wajibu wa serikali na upande wa pili, bunge likinukia harufu ya udikteta pale lilipofikiria kutumia jeshi kulazimisha uuzwaji wa mafuta katika vituo vya mafuta.
Hizo ni dalili tosha kuwa “maisha mabaya” kwa kila Mtanzania yanaipeleka nchi kwenye eneo gumu kiutawala. Unapoona msajili wa vyama vya siasa akijiingiza kichwakichwa katika kampeini za kubeza maandamano ya vyama vya siasa, ujue “maisha mabaya” kwa kila Mtanzania yamefika hata ndani ya ofisi ya msajili wa vyama vya siasa na kumfanya aache kuwa refa na kuwa mchezaji kamili wa siasa za vyama.
Ni vema tukajiuliza mpaka hapa, ni taasisi gani haijaguswa na “maisha mabaya” kwa kila Mtanzania. Jeshi la Polisi na Jeshi la Wananchi yaliingia mapema pale yalipoanza kutumiwa kama matawi ya chama tawala kutoa matamko elekezi.
Mahakama zilishirikishwa katika semina elekezi za watendaji wa serikali na kutoa viapo vya kuisaidia katika kukabiliana na wote wanaohoji kwa nini kuna “maisha mabaya” kwa kila Mtanzania.
Bunge ambalo ni chombo cha wananchi, limegeuka kuwa kama kinyonga. Mara tunaliona likitoa meno makali, lakini haichukui muda linanywea kama puto lililoishiwa pumzi.
Panahitajika kauli ya watawala juu ya tulipo sasa, kwa nini tuko hapa; wamekwama wapi na tuchukue hatua gani kuondoa “maisha mabaya kwa kila Mtanzania” ambayo yameingia katika kila kaya na maisha ya kila mmoja. Kunyamaza hakutaondoa chuki ya wananchi.

KAMA NI URAFIKI BASI HII NI KIBOKO